Friday, May 4, 2012

MAKABURI YA NUNGWI



Mwangwi wa vilio na simanzi kutoka kwa watu waliopoteza maisha baada ya meli kuzama kwenye mkondo wa bahari wa Nungwi, Zanzibar uliambaa kwenye maji na kwenda kugota kwenye ukuta wa chini ya bahari, mahali palipokuwa na maelfu ya makaburi yalichongwa kwenye mwamba mgumu kuhitimisha safari ya wote waliopoteza maisha yao kwenye ajali hiyo ya kihistoria.
 Kwa binadamu wa kawaida, wenye macho yanayoweza kutofautisha giza na mwanga pekee, hiyo ilikuwa ni ajali ya bahati mbaya kama zilivyo ajali nyingine lakini kwa wale wenye uwezo wa kuona zaidi  ya upeo wa  kawaida wa binadamu (beyond normal vision), haikuwa ajali ya bahati mbaya bali kitu kikubwa zaidi kilichopangwa na kuratibiwa kwa umakini wa hali ya juu.

“Babu! Mbona nasikia vilio vya watu wengi sana! Kwani kuna nini?” kijana mdogo anayefundishwa imani za kishirikina, Kahungo alikuwa akimuuliza babu yake.
“Hivyo ni vilio vya roho zilizopokonywa miili yao bila kujiaanda.“
“Unamaanisha nini babu?”


“Ili binadamu akamilike anapaswa kuwa na mwili na roho, vitu hivi vinapotengana, binadamu hufa. Sasa hawa wametenganishwa miili na roho ghafla kwenye ajali bila hata kujiandaa na ndiyo maana wanalia sana.”

“Sasa mbona wanazikwa wakiwa hai? Kwa nini wengine wanalia sana wakati wengine hawalii? Na hawa waliokuwa wanachimba makaburi huku chini ya bahari walikuwa wanatumia vifaa gani?”

Hawazikwi wakiwa hai. Zile unazoziona ndiyo roho, zinapambana kurudi kwenye miili yao inayoelea juu ya maji lakini zinashindwa. Wanaolia sana ni wale ambao kwenye maisha yao walimsahau Mungu na wakazama dhambini! Wale unaowaona hawalii ni wale ambao walikuwa wanafuata maagizo ya Mungu. Waliochimba makaburi haya ya Nungwi walitumia kitu chepesi sana, walitumia maarifa ya giza!”

“Maarifa ya giza? Lakini mbona hata misalaba inayowekwa kwenye makaburi haya siyo kama ile tuliyozoea kuiona kule duniani? Naona kama ni mifupa ya binadamu imefungwa na kutengenezwa misalaba,“ Kahungo alizidi kumhoji babu yake kwani kila alichokuwa anakiona kilikuwa kinamshangaza.
“Hizi ni kanuni za nguvu za giza! Mbona hushangai mimi na wewe kufika huku chini ya bahari bila ya kuwa mitungi  ya gesi wala nini na bado tunapumua kama kawaida?”

“Mh! Kweli dunia ina mambo. Halafu nilisikia kuna wazamiaji kutoka kusini mwa Afrika walishindwa kufika huku, mbona sisi tumefika kirahisi na bado naona watu wengi tu wakiendelea na shughuli za mazishi?”

“Hii dunia mjukuu wangu tunafaidi sisi wenye nguvu za giza! Hakuna kinachotushinda na ndiyo maana nataka nikuandae na wewe ufuate nyayo zangu, si unaona mimi nimeshakuwa mzee! Kuna kazi sana mpaka kufikia huku tulipo, unabidi uvuke ngazi nyingi sana. Wengi hata ngazi ya kwanza hushindwa kuivuka.”   

“Kwani hapa tulipo panaitwaje babu?”
“Nungwi! Kuna mkondo bahari wenye nguvu sana hapa na kuna wakati maji huwa yanachemka. Kutokana na maajabu ya hapa ndiyo maana wachawi waliamua kuweka kituo chao kikuu. Maji yanapishana kwa ngazi kuanzia juu hadi chini.

“Unataka kusema hiki ni kituo cha wachawi?”
“Eee! Wengi watashangaa kwa sababu ya ajali iliyotokea, lakini ukweli ni kwamba Nungwi ipo kwa miaka mingi iliyopita. Hii siyo ajali ya kwanza kutokea hapa. Mimi tangu nikiwa mdogo nilikuwa nakuja hapa kuongeza nguvu za kichawi na nilikuwa nikishuhudia ajali kubwa kuliko hata hii.”

 Maelezo ya babu yake yalimshangaza mno Kuhungo. Alizoea kusikia au kusoma hadithi za kutisha kwenye vitabu lakini sasa alikuwa eneo la tukio akishuhudia mwenyewe kila kitu. Babu yake akazidi kumfafanulia mambo.

“Siyo binadamu wote unaowaona duniani wanaishi kihalali, wengi hawafuati maagizo na mafundisho ya Mungu! Wanavunja amri zake kwa makusudi. Wanaabudu sanamu na kutukuza dhambi! Hawaogopi kufa wala adhabu za kaburi! Watu kama hawa wakiingia kwenye mitego ya nguvu za giza hawaponi!

“Sisi (wachawi) huwa tunasaidia kuwafikisha kwa urahisi kuzimu kwa kuwapitisha kwanza kwenye malago ya wachawi ambapo hutumikishwa kwa kipindi fulani kisha kuachwa waendelee na safari zao. Miongoni mwa njia za kuwasaidia wafike upesi kwenye safari zao ni kuwazika chini ya bahari.

“Babu! Unataka kusema makaburi chini ya bahari hayapo hapa Nungwi pekee?”
“Yapo sehemu nyingine nyingi, lakini kwa miaka mingi hapa ndiyo kwenye makaburi maarufu na mengi zaidi, ndiyo maana hata mkondo bahari wa hapa una nguvu kubwa na husababisha ajali nyingi na kubwa kuliko sehemu nyingine.”

“Aaah! Mbona unanichanganya! Kwani kilichoanza kuwepo hapa Nungwi ni makaburi ya chini ya bahari au mkondo wenye nguvu unaosababisha ajali?”

Swali lile lilimfanya yule mzee amkazie macho mjukuu wake huku akiwa ni kama ambaye hakutegemea kulisikia kutoka kwake. Aliachia tabasamu hafifu kisha akasema:

“Naona umekua siku hizi mjukuu wangu kwani unauliza maswali ambayo hata mimi nilipokuwa na umri kama wako sikuweza kuyafikiria. Kwa kuwa una hamu ya maarifa juu ya ulimwengu usioonekana kwa macho ya kawaida, nitakufafanulia kila kitu.”

“Cha kwanza kuwepo ilikuwa ni kituo kikuu cha wachawi miaka mingi sana iliyopita. Kutokana na nguvu za giza zinazozalishwa chini ya bahari kila wachawi kutoka sehemu mbalimbali wanapokutana, maji yalikuwa yakivurugika sana na kuchemka, ndiyo mkondo wa bahari ukaanza kutokea taratibu kisha ukawa unazidi kuongezeka nguvu.

“Mkondo huo ulianza kusababisha ajali nyingi kwa wasafiri wa majini na kupoteza maelfu ya roho za watu, waliokuwa wanakufa wakawa wanaletwa kuzikwa huku chini, ndiyo yakatokea makaburi haya ambayo yalizidi kuongezeka wingi kwa kadiri ajali zilivyokuwa zinazidi kutokea.”

Baada ya kukaa kule chini ya bahari kwa saa nyingi. Kahungo akishuhudia mauzamauza mengi ya kichawi, alimuomba babu yake waondoke kwani moyo wake ulishindwa kuvumilia yale aliyokuwa anayaona na kuyasikia. Wakashikana mikono na babu yake kisha wakafanya ishara za kichawi, Kahungo akaambiwa afumbe macho kama alivyofanya awali wakati wa kuja. Kufumba na kufumbua wakajikuta wako mchangani, ufukweni mwa bahari.

5 comments:

  1. naitaka yote hii hadisi ila sijui nifanyeje. maana kila niingia kuitafuta hua naipata kipandetu siipati kamili. nifanyeje mkuu nipe mbinu

    ReplyDelete
  2. Hongera Mkuu,ila Hata Mimi Naitaka Yote Sijuw Nifanyeje!

    ReplyDelete
  3. naitaka yote jaman naomba mwendelezo!!!!

    ReplyDelete